Daktari mmoja nchini Ufaransa ameweka rekodi ya dunia katika utabibu baada ya kufanikisha upasuaji uliofanikisha mwanaume mmoja wa kifaransa kupewa sura mpya kwa mara ya pili.
Bwana Jerome Hamon, chini ya uangalizi wa Dokta Laurent Lantieri alifanyiwa upasuaji uliohusisha yeye kupewa sura mpya mwaka 2010 katika hospitali ya Georges Pompidou ya jijini Paris.
Ilipofika mwaka 2015 Bwana Hamon alianza kusumbuliwa na sura yake hiyo mpya, ilianza kumkataa. Madaktari wamesema suala hilo lilisababishwa na dawa ambazo alitumia kipindi hicho zilizolenga kumtibu mafua makali.
Novemba mwaka jana (2017) seli za kibaiolojia za sura yake hiyo mpya zilianza kufa, seli (tissue) hizi ndizo zilizounganisha sura hiyo mpya na sehemu zingine za ndani ya uso wake. Suala hili likasababisha mahitaji ya sura hiyo kutolewa kabla madhara hayajawa makubwa zaidi.
Katika kipindi hicho uso huo ulipotolewa Bwana Hamon hakuwa na uwezo wa kuona, kusikia, wala kuongea au kula. Aliweza kusikia kwa mbali sana, na aliweza kuandika pale alipokuwa anahitaji chochote.
Bwana Hamon alifanikiwa kufanyiwa upasuaji wa pili wa kumpatia sura mpya mwezi Januari mwaka huu. Na ili kuhakikisha uso huo mpya uliopatikana kwa mtu mwingine aliyekuwa anakata roho utamkaa vizuri bila kumkataa hatua kadhaa za kitabibu zilichukuliwa. Moja ya hatua kubwa kabisa ni utabibu wa kipindi cha mwezi mmoja kabla ya upasuaji na kuwekea sura hiyo mpya ni kupatiwa damu mpya mwili mzima, damu iliyopitia kutibiwa kwa kipindi kirefu.
Uso wake wa kwanza, aliozaliwa nao, uliharibika kutokana na tatizo la kiafya alilonalo linalohusisha uso kuharibika kabisa.
Upasuaji wa kwanza wakati akiwa na umri wa miaka 35 ulimpatia uso wa mtu wa miaka 60, ila upasuaji huu kwa sasa akiwa na miaka 43 umempatia uso wa kijana wa miaka 22.
Vyanzo: Mitandao mbalimbali