Wanasayansi nchini Scotland wamefanikiwa kukuza kuku wenye uwezo wa kutaga mayai yatayokuwa na dawa ya kuimarisha mfumo wa kinga ya mwili na kutibu ugonjwa wa saratani.
Kwa mujibu wa vyanzo mbalimbali vya taarifa, Dkt. Lissa Herron na timu yake kutoka chuo cha teknolojia cha Roslin cha mjini Edinburg nchini Scotland, wamefanikiwa kuchanganya kinasaba cha binadamu na sehemu fulani ya kinasaba cha kuku inayohusika na kutengeneza ute mweupe wa yai kupata protini.
Mayai hayo yatakayozalishwa kutoka kuku hao yatakuwa na uwezo wa kuimarisha mfumo wa ulinzi wa binadamu na kutibu magonjwa kama saratani. Utengenezaji wa dawa kwa njia hii utashusha gharama ya kutengeneza dawa hizo hadi mara 100 ukilinganisha na uzalishaji wa dawa za ugonjwa wa saratani kutoka viwandani.