Mauzo ya simu janja za Huawei yaporomoka kwa asilimia 40. Zuio la biashara la Marekani limeanza kuleta athari za kimapato kwa Huawei baada ya data zao kuonesha kuporomoka kwa mauzo ya simu ukilinganisha na kipindi cha mwenzi mmoja uliopita.
Hayo yamesemwa na mwanzilishi wa kampuni hiyo Bwana Ren Zhengfei na baadae taarifa hiyo kukubaliwa na msemaji wa kampuni hiyo.
Huawei wamesema asilimia hiyo ya kudondoka kwenye mauzo imesababishwa na hatua ya Marekani kuiwekea vikwazo vya kibiashara ambavyo hadi sasa vimeathiri mahusiano ya kibiashara kati ya kampuni mbalimbali ikiwa ni pamoja na Google, Facebook, Intel, Microsoft na wengine wengi.
Wamesema katika soko lao la ndani – yaani nchini China bado mauzo yanaendelea vizuri bila athari yeyote. Hii inaweza isishangaze kwani simu zinazouzwa nchini humo hazina apps mbalimbali ambazo zishazoeleka nje ya China – hii ikiwa ni pamoja na Google Playstore, Gmail, Google Maps, WhatsApp, Facebook, Instagram na apps nyingine mbalimbali za mitandao ya kijamii za mataifa ya magharibi.
Huawei waliingiza sokoni simu janja milioni 206 mwaka 2018, takribani nusu ya simu hizo zikibakia nchini China na nusu yake kuuzwa mataifa mengine.
Bwana Ren amesema wanategemea kupunguza uzalishaji wa simu katika kipindi cha hadi miezi 24 kuweza kuelewa hali ya soko. Wanategemea mapato yatashuka kwa asilimia hadi 30 kwa mwaka huu, akiwa na mategemeo kufikia mwaka 2021 wataweza kuanza kukua tena.
Watafiti wengine wa masoko wanaamini mauzo hayo yanaweza yakaja kushuka kwa kati ya asilimia 40 hadi 60 ndani ya kipindi cha mwaka mmoja.
Kufahamu kwa undani sakata hili unaweza pia kusoma habari zifuatazo tulizoziandika hapa Teknokona;
- Simu za Huawei kukosa Google Playstore na huduma zingine za Google
- Huawei wana programu endeshaji (OS) yao kwa ajili ya simu na kompyuta
- Tetesi: Toleo la Android la Huawei lina kasi ya 60% zaidi ya toleo la Google
- Intel waitetea Huawei: Nje ya Google fahamu makampuni mengine yaliyoathirika