Mtandao maarufu wa Telegram mwishoni mwa wiki ulipotea takribani dunia nzima baada ya kupata joto kali zaidi katika server zao hivyo kupelekea kushindwa kufanya kazi kama ilivyo kawaida yake.
Muanzilishi na mkurugenzi wa Telegram, Bw. Pavel Durov alitoa taarifa kwa umma kwamba hali hiyo ilitokana na shambulizi la kimtandao lililoikumba Telegram. Hali hiyo ilidumu kwa takribani saa mbili kwa nchi kadhaa na kwa baadhi ya nchi tatizo hilo liliendelea kwa zaidi ya saa mbili.
Kutokana na hali hiyo watumiaji wengi wa Telegram walipatwa na fedhea kubwa kwa kushindwa kufanya chochote kupitia App hiyo ambapo hakuna aliyekuwa anajua nini kimeitokea Telegram.
Wakati wa tatizo hilo mtumiaji wa Telegram kila alipojaribu kufungua programu hiyo tumishi ilikuwa inampa maelezo aidha connecting……. na kumfanya asiweze kufanya chochote. Baadhi ya maeneo mengine iliweza kufungua vizuri lakini asiweze kutuma au kupokea ujumbe wowote.
Kwa muda sasa Telegram imekuwa kwenye mzozo na serikali ya Urusi baada ya kugoma kutoa fursa ya kwa shirika la ujasusi la nchini humo, FSB kuwa na uwezo wa kuingia kwenye server za Telegram kuchunguza matukio ya kigaidi.
Kutokana na kukaidia agizo hilo, serikali ya Urusi imechukua maamuzi ya kuipiga marufuku Telegram nchini humo jambo ambalo linaangaliwa kama kuingilia uhuru wa watu katika usiri wao.