Miezi michache iliyopita kuna teknolojia ya nchini China ilijipatoa umaarufu sana, ilikuwa teknolojia ya mabasi yanayoruhusu magari mengine kupita chini yake. Teknolojia hii inalenga kupunguza uhitaji wa njia spesheli kwa mabasi ya mwendokasi.
Soma zaidi: Basi linalopita juu ya magari lafanyiwa majaribio China.
Na sasa miezi kadhaa mbele kampuni inayohusika na teknolojia na utengenezaji wa mabasi hayo imejikuta kwenye skendo kubwa ya ufisadi na hadi sasa mchakato mzima wa utengenezaji wa mabasi hayo umekwama.
Teknolojia hiyo ilipewa jina la TEB – Transit Elevated Bus, inajumuisha mabasi yanayotumia umeme yenye uwezo wa kubeba abiria hadi 300 na huku ikitembea kwenye njia yake spesheli inayokuwa pembeni (pande mbili) ya barabara inayotumiwa na magari madogo chini huku mabasi hayo yakiruhusu sehemu kwa chini magari madogo kuweza kupita.
Kampuni ya utengenezaji, Huaying Kailai, ilifanikiwa kufanyia majaribio ya teknolojia hiyo mwezi wa nane mwaka jana katika jiji la Quinghuangdao na umaarufu wake ukasambaa duniani kote.
Ila hadi sasa tayari serikali ndogo ya jiji hilo imesema itaondoa njia za basi hilo. Kwa kifupi mradi mzima umekwama na kampuni husika imejikuta chini ya uchunguzi wa kifisadi huku ikitakiwa kurudisha mamilioni ya pesa iliyochukua kwa watu na mashirika yaliyofanya uamuzi wa kuwekeza katika kampuni hiyo.
Inasemekana njia waliyotumia kupata pesa za uwekezaji haikuwa njia inayotambulika kisheria. Inasemekana pesa hizo zilipokelewa kupitia tovuti moja nchini humo na hadi sasa viongozi wake wanashikiliwa katika kusaidia polisi ili kufanikisha kurudisha pesa
Inasemekana kampuni ya Huaying Kailai ilichukua kiasi cha pesa kutoka kwa wawekezaji kinachokaribia dola bilioni 1.3 za Kimarekani (Kumbuka dola 1 ni takribani Tsh 2,200/=).
Polisi nchini China kwa sasa wameweka suala la utapeli wa aina hii kipaumbele katika vita dhidi ya ufisadi, watu wengi nchini China kila mwaka wanavutiwa kuwekeza katika bidhaa mbalimbali ambazo mwisho wa siku utengenezaji wake unashindikana na pesa zao zinapotea.
Video inayoonesha mfumo mzima wa mabasi hayo ambavyo ungefanya kazi;
Je tutakuja kuona mabasi ya aina hii?
Hakimiliki ya teknolojia hii bado inamiliki na kampuni hii na kwa kuwa washaweza hadi kutengeneza mfano – prototype, basi tusishangae kuona leseni ya teknolojia hii ikinunuliwa na makampuni mengine na mabasi ya namna hii kuanza kutumika miaka mingine baadae.
Soma zaidi: Basi linalopita juu ya magari lafanyiwa majaribio China.