Kiwanda cha kutengeneza simu kuanzishwa nchini Rwanda. Waziri wa sayansi, teknolojia na mawasiliano nchini Rwanda, Paula Ingabire amesema kwamba tayari mazungumzo yameanza na sekta binafsi kwa lengo la kuanzisha kiwanda cha kwanza cha utengenezaji wa simu za kisasa.
Kulingana na taarifa zilizotolewa na vyombo vya habari nchini Rwanda, kiwanda hicho itakuwa ni hatua kubwa katika sekta ya teknolojia na mawasiliano katika ulimwengu wa kisasa ambao umekuwa kama kijiji kimoja.
Kampuni iitwayo Mara itashirikiana na serikali ya Rwanda katika utengenezaji wa simu za bei nafuu kwa wananchi wa Rwanda.
Simu za Mara X zitakuwa zikitengenezwa katika viwanda nchini Rwanda na Afrika Kusini. Kampuni ya Mara Group imesema ina malengo ya kuwa na viwanda mataifa kadhaa Afrika.
Mpango huo uliwekwa wazi Alhamis iliyopita na Waziri Paula Ingabire wakati akiwa mbele ya kamati ya Bunge ya elimu, Teknolojia, Utamaduni na vijana akizungumzia masuala ya ICT.