Kaspersky Lab marufuku serikalini. Serikali ya Marekani chini ya uongozi wa Rais Trump imepiga marufuku utumiaji wa programu ya antivirus maarufu ya kuzuia virus na mashambulizi ya data kwenye kompyuta ya Kaspersky na huduma zingine zote kutoka kampuni hiyo.
Janga hili limeikuta kampuni ya Kaspersky Lab, watengenezaji wa Antivirus ya Kaspersky, kama muendelezo wa tuhuma zinazofanyiwa uchunguzi juu ya Serikali ya Urusi kushiriki utumiaji wa mtandao katika kushawishi matokeo ya uchaguzi wa Urais uliopita.
Kwa nini janga hili limeikuta Kaspersky?
Kampuni ya Kaspersky makazi yake makuu ni nchini Urusi. Mwanzilishi mkuu wa shirika hilo maarufu duniani, Bwana Eugene Kaspersky ambaye pia ni Mkurugenzi Mkuu ni raia wa Urusi.
Kaspersky Lab ni moja ya kampuni nguli sana katika masuala ya usalama wa data za kikompyuta na sifa hii imeiwezesha kupata mikataba mizuri ya kutoa huduma za kiusalama za kompyuta kwa Serikali nyingi ata nchi za Magharibi kama vile Marekani.
Kwa Marekani huduma zao zimekuwa ni muhimu sana hadi kuwafanya kuwa na ofisi spesheli kwa ajili ya kuhudumia serikali hiyo. Ofisi hii kwa sasa imefungwa baada ya serikali ya Marekani kutoa onyo kwa wizara zake zote.
Wizara ya Mambo ya Usalama ya nchini humo (Department of Homeland Security) imezipa taarifa ofisi za serikali nzima ya Marekani ya kwamba wanatakiwa kuzitambua huduma zote za Kaspersky Lab wanazozitumia ndani ya siku 30 na kisha kuhakikisha ndani ya siku 90 huduma hizo zimesitishwa na watamie nyingine mbadala.
Kaspersky wamefanya nini?
Mkurugenzi Mkuu bwana Eugene Kaspersky ameomba kupatiwa hati ya dharula ya kumruhusu kuingia Marekani (Visa) ili aweze kuhojiwa na kamati ya bunge la Marekani inayohusika na uchunguzi juu ya Urusi.
Bwana Kaspersky ameshikilia msimamo wa kwamba kampuni hiyo haijihusishi vyovyote na uvunjifu wowote wa sheria za Marekani na inachukulia shutuma zingine zote kuhusu wao ni kwa sababu tuu kampuni hiyo makazi yake makuu ni Urusi.