Kampuni tisa kati ya 12 bora za utengenezaji wa simu rununu duniani zina makao yake makuu nchini Uchina zikiwemo za Huawei, Oppo, Vivo na Xiaomi hiyo ikiwa ni kwa mujibu wa orodha ya wazalishaji bora mwaka 2017 kigezo kikubwa kikiwa ni mauzo ya bidhaa hizo.
Kwa mujibu wa orodha iliyotolewa hivi karibuni na kampuni ya IC iliyopo Arizona, Marekani, na ambayo hushughulikia tafiti na masoko kwa wazalishaji wa bidhaa za kielektroniki, ni kampuni tatu tu zisizokuwa za Uchina kuwamo kwenye kumi na mbili bora, ambazo mbili kati ya hizo ni Samsung na LG za Korea Kusini na nyingine ni Apple ya Marekani.
Aidha, orodha hiyo inaonyesha kuwa Huawei, Oppo, Vivo na Xiaomi ndiyo kampuni nne pekee zilizoongeza mauzo ya simu zake kwa kiwango cha asilimia zaidi ya moja.
Miongoni mwa kampuni hizo, Xiaomi ndiyo kinara wa mauzo kwa mwaka uliopita baada ya kuwa na ongezeko la asilimia 73.
Orodha kamili ya kampuni 12 zinazoongoza kwa mauzo ya simu zake ni kama ifuatavyo:
- Samsung (Korea Kusini)
- Apple (Marekani)
- Huawei (Uchina)
- Oppo (Uchina)
- Vivo (Uchina)
- Xiaomi (Uchina)
- LG (Korea Kusini)
- Lenovo (Uchina)
- ZTE (Uchina)
- TCL (Uchina)
- Gionee (Uchina)
- LeEco/Coolpad (Uchina)
Wakati huo huo, kampuni nyingine tatu za Kichina — LeEco/Coolpad, ZTE na TCL – zilikumbwa na janga la kuporomoka kwa mauzo ya simu zake kwa kiwango cha zaidi ya asilimia 20 katika kipindi cha mwaka uliopita.
Kwa mujibu wa takwimu za orodha hiyo, kwa pamoja, kampuni tisa vinara za Uchina ziliuza simu janja milioni 626 mwaka 2017, ikiwa ni ongezeko la asilimia 11 kulinganisha na simu milioni 565 zilizouzwa na kampuni hizo tisa mwaka 2016.
Na kwa ujumla, soko la dunia la simu lingali likishikiliwa kwa kiasi kikubwa na kampuni za Uchina zilizoshikilia asilimia 42 ya soko lote la dunia mwaka 2017, hiyo ikiwa ni ongezeko kubwa zaidi kulinganisha na asilimia 38 ya mwaka 2016 na asilimia 34 ya mwaka 2015.
Hata hivyo, taarifa ya ripoti hiyo ilionyesha kuwa Samsung na Apple ndio zinazoshikilia soko la simu rununu ghali zaidi duniani – bei za bidhaa zake zikiuzwa kila moja kuanzia dola za Marekani 200, sawa na Tsh. 440,000).