Wakazi wa Jiji la Mwanza na Manispaa ya Ilemela tarehe 02/05/2019 wameanza rasmi kutumia mfumo mpya wa Kielektroniki wa malipo ya ushuru wa maegesho ya magari (TARURA e-PARKING) ambao unatumia mfumo wa kielektroniki wa malipo ya serikali yaani Government Electronic Payment Gateway (GePG).
Lengo la TARURA kutumia mfumo wa Kielektroniki ni kuongeza ufanisi wa ukusanyaji wa mapato ya serikali ili kuboresha miundombinu ya barabara za vijijini na mijini. Mfumo huu (TARURA e-PARKING) ni rahisi na salama ambapo mtumiaji wa maegesho yaliyo kwenye hifadhi ya barabara za TARURA anapaswa kulipia maegesho kwa kutumia simu yake ya mkononi, benki au wakala na pesa atakayolipa inakwenda moja kwa moja kwenye akaunti ya serikali.
Faida ya kuanzisha na kutumia mfumo huu utampunguzia mtumiaji wa maegesho kero ya kudaiwa ushuru wa maegesho na kufungiwa chombo chake cheni, kwani mtumiaji atalipa mwenyewe kwa kutumia simu yake ya mkononi, wakala au benki. ili, mfumo husika utasaidia kuboresha mipango ya barabara na kupunguza changamoto za maegesho ya chombo cha moto.
Mteja analipaje? Malipo yanaweza kufanyika kwa njia mbili tofauti…..
Kwanza unatakiwa upate kumbukumbu namba ya malipo ambayo utaipata kwa kubonyeza *152*00# kisha fuata maelekezo. Utachagua namba 4 (Nishati na Usafiri), kisha chagua namba 2 (TARURA e-Parking), utachagua namba 1 (kulipia maegesho), ingiza namba ya chombo, chagua mkoa, chagua eneo la maegesho, chagua aina ya chombo. Kisha utapokea ujumbe mfupi wenye kumbukumbu namba na kiasi unachotakiwa kulipia maegesho ya magari.
Hatua ya pili baada ya kupata kumbukumbu namba (control number) unalipia maegesho kwa kutumia mitandao yote ya simu T-Pesa, M-Pesa, Airtel Money, Tigopesa, Halopesa, Ezypesa unalipa kwa wakala yoyote au kwa kutumia tawi lolote la benki.