Wajapani kama vile wazungu, wanapenda sana kutumia kibanika mkate kwenye kuandaa mikate yao. Tendo la kubanika mkate (yaani toast) ni la umuhimu sana kwao kiasi kwamba kampuni moja imekuja na mashine inayouzwa kwa bei ya zaidi ya nusu milioni.
Kwa miaka kadhaa sasa nchini Japani na mataifa mengine kumekuwa na umaarufu wa vifaa vipya vya kisasa vya ubanikaji mikate.
Kifaa cha ‘toaster’ kina kazi moja tuu – kuchoma mkate katika ubora/kiwango flani, na kutumia zaidi ya laki 6 katika ununuaji wa kifaa kama hicho kwa wengine inawezekana ikawa ni utumiaji mbovu wa pesa. Kwa wapenda mikate inayopitia hatua hii pesa hii inaweza kuwa ni jambo la kawaida tuu, tayari kuna vifaa hivyo vingine vinavyouzwa kwa bei karibia na hiyo.
Kibanika mkate hiki kimetengenezwa na kampuni ya Mitsubishi – Mitsubishi Electric Corp. Ingawa mara nyingi vifaa hivi vinakuwa na uwezo wa kupokea zaidi ya kipande kimoja cha mkate, machine hii imepewa uwezo wa kupokea kipande kimoja tuu.
Wenyewe Mitsubishi wamesema wamefanya hivyo ili kuhakikisha ubora wa hali ya juu katika kipande kimoja – kuliko kuwa na uwezo wa kupokea vipande vingi huku ubora ukiwa si mzuri.