Ujio wa toleo la iPod Touch la mwaka 2019 unaleta ujumbe mkubwa sana uliojificha. Ujumbe huo ni kwamba Apple kwa sasa wanawekeza kwenye ‘huduma zaidi’, wameshaona mapato kwa njia ya kuuza iPhone tuu yanashuka ila ni huduma zake za kwenye iOS ndio zinatengeneza pesa.
Kwa muda sasa suala la mauzo la simu za iPhone limeonesha khuwa changamoto kwa Apple. Wamepandisha bei sana kwa matoleo ya simu zao za hivi karibuni. Katika kipindi hicho hicho soko la simu duniani halijakuwa na ukuaji na pia makampuni mapya ya simu kwa bei nafuu zaidi ya Apple tena zenye uwezo mkubwa yameingia sokoni: hii inajumuisha One Plus, Xiaomi, na mengine mengi.
Apple wamejikuta katika wakati mgumu kwani mauzo ya matoleo mapya ya simu yameporomoka kufikia hatua ya kuacha kutangaza mauzo ya simu zao ukilinganisha na zamani. Kwa sasa Apple wanawekeza zaidi kwenye huduma ambazo wanaziuza kwenye watumiaji wa programu endeshaji yao ya iOS.
Na suala hili linaonekana zaidi kwa ujio wa iPod Touch zao mpya kwa mwaka 2019. iPod Touch hii inauwezo mkubwa wa kiutendaji wa kufaninishwa na simu zao za kisasa kama vile iPhone 7 ma 8 lakini inapatikana kwa bei nafuu sana ukilinganisha na bei za simu hizo: kwa bei inayoanzia dola 199 za Marekani (Takribani TSh 460,000).
Kitu pekee kinachokosekana katika iPod Touch ukilinganisha na simu kama iPhone 7 ni suala la uwezo wa kupiga picha, utambulizi wa sura (facial recognition) katika ufunguaji simu.
Sifa na bei za iPod Touch:
- Processor:Inatumia prosesa ya kisasa kabisa kutoka Apple ya A10 Fusion ambayo ipo pia kwenye simu za iPhone 7 na iPhone 7 Plus. Prosesa hii itahakikisha vitu kama vile magemu yanacheza kwa ubora mkubwa.
- Diski uhifadhi: Inapatikana katika diski uhifadhi wa GB 32, GB 128, na GB 256
- Ukubwa/Upana: Inaukubwa wa mm 123.4 kwa mm 58.6mm, huku wembamba wake ukiwa mm 6.1, na uzito wa gramu 88.
- Kioo/Display: Inchi 4, ikiwa na kiwango cha ubora wa 1136 x 640
- Headphone Jack: Wakiwa wameshaacha kuweka eneo la kuingizia earphone kwenye iPhone zake zote za siku hizi, hali ni tofauti kwa iPod Touch. Sehemu hiyo inapatikana.
- Programu endeshaji: Inakuja na toleo la iOS 12, ila itapata masasisho ya matoleo mapya ya iOS wakati mmoja na simu za iPhone. Toleo la iOS 13 linategemewa baadae mwaka huu.
- Kamera: Kamera kuu ni ya megapixel 8 (aperture f/2.4), HDR & Auto Image Stabilization, 1080p HD. Kamera ya selfi ni ya megapixel 1.2 (aperture f/2.2), 720p HD.
Kuhusu bei ujazo wa GB 32, inapatikana kwa bei takribani Tsh 460,000/= za kitanzania, huku GB 128 ikiwa Tsh 690,000/= na GB 256 ikiwa ni Tsh 920,000/=. Kumbuka ingawa iPod Touch inasifa na kutumia apps nyingine zote kama vile iPhone ni sifa moja inakosekana kwenye iPod Touch. Nayo ni kutokuwepo kwa uwezo wa kutumia kadi ya simu.
Kwa huduma za intaneti iPod Touch inatumia WiFi pekee. Kwa kifupi inalenga watu wanaotaka kuwa na kifaa kwa bei nafuu kwa ajili ya matumizi ya huduma kama vile muziki, kucheza magemu (toleo hili linakuja na teknolojia za kisasa kabisa za 3D) na kutazama filamu. Kumbuka bado mtu atakuwa na uwezo wa kupata apps zote zinazopatikana kwenye iPhone pia kupitia soko la apps la AppStore.