Tukiangazia teknolojia za karibuni kabisa makampuni mengi yamekuwa yakiweka jitihada nyingi tu kuhakikisha kuwa simu janja wanazozileta sokoni basi zinakuwa na uwezo wa kutunza chaji kwa muda mrefu hata kuwa na mbadala wa kuweza kuchaji kitu kingine.
Mwaka 2019 tutaweza kuona bidhaa za Apple zikifuata nyayo za Samsung na Huawei kuhakikisha wateja wao hawahitaji kubeba vimemeshi vya aina tofauti kwani kifaa kimoja kina uwezo wa kuchaji vingine na kwa hakika hii ni habari njema kwa dunia ya leo.
Teknolojia inayowezesha simu janja kuweza kuchaji vitu vingine.
Tukirudi nyuma mwaka 2015 ndio ilitambulishwa teknolojia inayowezesha simu janja kuweza kuchaji vitu vingine kwa lugha ya Kiingereza tunasema Wireless PowerShare. Hivyo basi simu kama Huawei Mate 20 Pro, Samsung Galaxy S10 zina kipengele hicho ambacho kinawezesha kuchaji vitu kama Galaxy Watch bila kutumia kimemeshi chake halisi. Baadae mwaka huu simu za iPhone zitakuwa na uwezo wa kuchaji vitu kama Apple Watch, AirPods toleo jipya.
Hatua hii inaonekana kuwa nzuri hasa kwa wale ambao hatupendi kubeba vimemeshi vya aina tofauti tofauti ili kuweza kuchaji bidhaa nyingine za kidijitali na hili linaweza likavutia watu wengi kuweza kununua iPhone toleo linalokuja mwishoni wa majira ya joto.
Vyanzo: GSMArena, Slash Gear