Je umeshtuka baada ya kusoma kichwa cha habari hichi; Hyundai Waja na Gari Linalotembea Kama Roboti…? Usihofu ukuaji wa teknolojia utatuletea vichwa vya habari vingi vitakavyotushtua.
Kuna filamu maarufu zinazokwenda kwa majina ya Transformmers, katika filamu hizo magari yanabadilika na kuchukua maumbo ya kiroboti huku yakiweza kutembea kwa miguu.. kwa kiasi flani Hyundai wanataka fanikisha kiasi kidogo cha kilicho kwenye filamu hizo.
Kampuni nguli ya magari ya nchini Korea Kusini, Hyundai, wametambulisha programu yao ya utengenezaji wa gari linaloweza kutumiwa vizuri katika maeneo yenye majanga ya kimazingira yanayoharibu miundo mbinu muhimu kama barabara.
Gari linaloenda kwa jina la Hyundai Elevate linaletegemewa kuwa gari bora zaidi kwa ajili ya timu za uokoaji na usambazaji wa mahitaji muhimu katika vipindi vya majanga.
Gari la Hyundai Elevate linaweza kuendeshwa kwa matairi manne kama kawaida, ila pale inapohitajika basi eneo la matairi hayo litafunguka na umbo la miguu badala ya matairi litatokea. Baada ya hapa gari litatembea miguu kama vile ya mdudu buibui (kimombo spider).
Katika mfumo huu inaweza kuwa rahisi kwa gari hilo kupanda milima, kupita maeneo yenye mawe au yasiyopitika kwa urahisi – nje ya hapo linaweza hadi kupanda ukuta mfupi kama wa futi tano. Gari litatembea kwa miguu minne kama vile mdudu buibui.
Gari hilo linatumia umeme, na kupitia chesis yake kuna mabetri kadhaa yamepangwa kulihakikishia umeme wa kutosha pale linapoitajika kufanya kazi.
Tazama video fupi ya gari hili hapa chini na utuambie mtazamo wako juu ya teknolojia hii.