Huawei inapitia katika kipindi kigumu kuweza kufanya kazi hasa nchini Marekani kutokana na kuwepo kwa “Vuta nikuvute” kati ya nchi hizo mbili na tayari kampuni hiyo ya Uchina inafahamu ugumu inaoupitia ingawa Google wamesema wataendelea kushirikiana na Huawei katika kipindi cha miezi mitatu ijayo.
Tunafahamu vyema kuwa Google ilitangaza kuacha kuacha kufanya kazi na Huawei jambo ambalo limewahuzunisha wateja/wanaomiliki rununu za Huawei na kimsingi ndio wanaoumia lakini sasa Marekani imesema imeiruhusu Huawei kuendelea kutoa huduma kwa watu wa nchi hiyo kwa siku tisini. Baada ya taarifa hiyo kutoka watu wakawa wanaitazama Google iwapo nao watarudisha nyuma walichokisema hapo awali.
Google wataendelea kutoa masasisho ya ulinzi kwa programu endeshi (Android), kuwepo kwa soko la programu tumishi/PlayStore kwa simu za Huawei mpaka Agosti, 19 2019.
Nini kitatokea baada ya siku 90 kupita?
Baada ya miezi mitatu kutimia, simu janja za Huawei zitazotoka kuanzia Agosti, 19 2019 hazitakuwa na programu tumishi kama Youtube, Gmail, kivinjari cha Google, soko la programu tumishi, kupokea masasisho ya kuimarisha Android lakini ambacho Google hakina uwezo wa kufanya ni kuzuia simu za Huawei kutumia programu endeshi-Android kutokana na kwamba Android ni programu endeshi ya wazi ambapo yeyote anaweza kuiboresha/kuitumia kwa lugha rahisi leseni ya programu endeshi husika ni HURIA!.
Hayo ndio mambo ya Google inayoonekana kufuata agizo la serikali ya rais Trump dhidi ya Huawei inayoonekana kuwa ni tishio kwa watu wa Marekani kiasi kwamba hata mataifa mengine duniani kutia shaka na huduma zao hasa ya 5G.
Vyanzo: Phone Arena, CNET