Binance, moja ya kampuni kubwa inayojihusisha na kusimamia akiba na mihamala ya pesa ya kidigitali ya Bitcoin imedukuliwa na mabilioni ya pesa – dola milioni 41 za Marekani – takribani zaidi ya bilioni 80 za kitanzania.
Fedha za mfumo wa kidigitali, Bitcoin, bado una watumiaji wengi duniani kote.
Watu wengi wamewekeza na kuhifadhi pesa zao katika mfumo wa pesa za kidigitali wa bitcoin wakiamini ni njia nzuri ya kuhifadhi pesa huku wakiwa na mategemeo ya pesa hiyo kupanda thamani mbeleni. Umaarufu huu wa mfumo wa pesa za kidigitali ambazo zinaweza kutumiwa pia kwa mihamala mbalimbali mitandaoni umesababisha pia suala la wizi wa udukuzi kuanza kukua.
Inasemekana kwa kutumia njia mbalimbali hasa hasa za kudanganya hatua kadhaa za kiusalama kama vile kubadilisha nywila (passwords) n.k, wadukuzi hao waliweza kupata taarifa za ‘wallet’ – hifadhi, ya pesa hizo za kidigitali zilizokuwa chini ulinzi mkubwa wa kiteknolojia.
Kampuni ya Binance, iliyopatwa na janga hilo imesema wadukuzi hao wamekwapua waleti ya kidigitali iliyokuwa inawakilisha asilimia 2 ya hifadhi zote za Bitcoin. Kwa bahati yao tayari walikuwa na bima itakayohakikisha pesa hizo zitawarudishwa kwa wateja wao bila shida yeyote.
Hii si mara ya kwanza kwa matatizo kama haya kutokea kwenye biashara za pesa hizi za kidigitali. Hivi karibuni kampuni nyingine ilijikuta ikipata hasara za mabilioni baada ya mtu pekee mwenye nywila ngumu za mfumo wa usalama wa kidigitali wa pesa kufa ghafla na huku hakukuwa na mtu mwingine yeyote mwenye taarifa za kufungua mfumo huo.
Biashara ya fedha za kimtandao za Bitcoin ina changamoto nyingi sana – nyingine ikiwa ni pamoja na uporomokaji wa ghafla wa thamani ya pesa hiyo. Watafiti wengi wanaona ata kama fedha hii itaweza kudumu basi itachukua miaka kadhaa kuweza kuwa na thamani yake halisi.