Azam TV kuanza kuonesha chaneli za ndani bure ndani ya kipindi cha miezi 7. Wizara ya Ujenzi, Uchukuzi na Mawasiliano imetangaza kuwa Kampuni ya Azam tayari imepewa leseni kutoka Mamlaka ya Mawasiliano Tanzania inayoruhusu kurusha matangazo ya chaneli za bure.
Hayo yamesemwa na Naibu Waziri wa Wizara ya Ujenzi, Uchukuzi na Mawasiliano Mhandisi Atashasta Justus Nditiye kwamba Jumatatu ya wiki hii Azam imepata leseni ya kuruhusiwa kuonesha chaneli za Bure.
Waziri Mhandisi Atashasta Justus Nditiye aliyasema hayo Jumanne Bungeni katika kipindi cha maswali na majibu wakati anajibu swali la nyongeza la Mbunge wa Mlalo Mh Rashidi Shangazi.
Azam wameahidi ndani ya miezi saba watakuwa wamejenga mfumo wa kurusha chaneli hizo eneo lote la nchi.
Teknolojia inayoruhusu urushaji wa chaneli kwa mfumo wa bila malipo unategemea sana uwekezaji wa vituo vya urushaji wa data katika maeneo ya ardhini.
Awali Ving’amuzi vya AZAM TV, ZUKU na DSTV vilizuiwa kuonesha channeli za ndani kwa sababu leseni zao walizoomba na kupewa hazikuwa zinaruhusu kuonesha chaneli hizo.
Hata hivyo suala la kuanza kuonekana kwa Chaneli hizo kutahitaji muda wa miezi kadhaa mpaka kukamilika kwa zoezi la kutandaza mfumo wa kuonesha chaneli za Bure nchi nzima.