iOS ambayo ndio programu endeshi inayoitambulisha bidhaa za Apple kwa ulimwengu imekuwa mstari wa mbele kutoa masasisho mara kwa mara au hata kurekebisha kitu ndani ya muda mfupi sana, sasa baada ya iOS 11 ya 12 imeingia.
Kuboresha kitu kutokana na sababu mbalimbali ni kitu muhimu sana au hata kuwa uti wa mgongo kuweza kupiga hatua moja kwenda nyingine na kwenye biashara yenye ushindani kama vifaa vya teknolojia kufanya kitu kionekane kipya kila baada ya muda fulani ni muhimu kweli kweli.
iOS 11 ambayo imedumu kwa muda wa mwaka mmoja tu, Apple wametoa toleo la 12 Juni 4 2018 ambalo limekuja likiwa limeangazia zile kasoro ambazo zililalamikiwa sana kwenye toleo lililopita yaani iOS 11.
Vitu vya kuvutia/vilivyoboreshwa kwenye iOS 12.
>Kasi. Kasi kwenye vifaa vya kidijiti (simu, kompyuta, n.k) ndio kiini cha kupata sifa za kwanza kabisa. Kwenye iOS 12 upande wa kamera inafungua 70% haraka zaidi tofauti na mwanzo. Vitu kama kicharazio, uso wa mbele wa iOS 12 unafunguka kwa haraka nusu ya ule muda kwenye toleo lililopita.
>Taarifa fupi. Kwenye toleo la iOS 11 taarifa fupi zilikuwa zinaonekana kila moja kivyake lakini mambo ni tofauti kwenye iOS 12 kwani taarifa zote za kutoka kwenye programu tumishi zinakusanywa na kuwekwa katika kundi moja.
Uraibu wa matumizi ya simu. iOS 12 imekusogeza karibu kabisa na kuweza kujua wewe unapendelea kutumia muda kiasi gani kwenye programu fulani ya kwenye simu yako. Mbali zaidi unaweza ukaweka muda wa kusitisha kupokea taarifa fupi kutoka kwenye programu tumishi/kipengele husika.
“Weka mbali na watoto”. Mtoto wako nae unaweza ukawa unapata taarifa zake kuhusiana na uraibu kwa upande wake na hata kuweza kusitisha yeye (mtoto) kupata taarifa fupi kutoka kwenye WhatsApp, Instagram, n.k kwa muda utakaouweka kupitia simu yako.
>Usalama & Faragha. Apple wamekuwa mstari wa mbele kuhakikisha hata kama kifaa chako kikiibiwa basi kisiweze kutumia na mtu mwingine. Kipengele cha USB Time Out kipo kwenye iOS 12 ambacho kazi yake ni kupunguza vitu vinavyoweza kufanyika kwenye simu hiyo baada ya simu/kifaa hicho kutokuwa hewani kwa muda wa saa moja.
Hii itafanya kuweza kufanya vitu vichache sana iwapo mtu atajaribu kuidukua/kuunganisha kwenye kompyuta. Vile vile toleo la iOS 12 linazuia Facebook pamoja na mitandao minigne kuweza kukufuatilia bila ya ridhaa yako.
>Kunakili tarakimu maalum za uhakiki. Kwenye iOS 12 imeondoa ile tabia ya kwenda kunakili zile namba maalum za kuhakiki kama kweli ni akaunti yako (two/one way factor) na ilichokifanya ni kunakili mara moja tu huku mara nyingine zote ikizijaza zenyewe bila ya mtumiaji kwenda sehemu zilipo kuzinakili tena.
Njia fupi za kutumia kwenye iPad. Unaweza ukawa ni mpenzi wa kutumia njia ambazo si ndefu kuweza kufika sehemu husika; iOS 12 kwenye iPad inakuwezesha kupangusa chini kwenye kingo ya upande wa kulia kufika kwenye control centre au upanguse kwenda chini kutoka kingo ya upande wa kushoto kupata taarifa fupi. Vilevile, ukipangusa kwenda juu utapata kipengele cha dock na ukirudia tena kupangusa kwenda juu utarudishwa kwenye uso wa mbele (nyumbani).
>SIRI na mambo yake. Kwenye iOS 12 unaweza ukaweka kifupisho chako mwenyewe kwa ajili ya kufanya kitu fulani kwenye SIRI.
>Picha. Usishangae kuona kipengele cha “For You” kwenye uwanja wa picha. Kipengele hiki kazi yake ni kutoa mapendekezo kushirikisha watu wengine ambao wapo kwenye picha husika.
>Vikatuni vinavyochezacheza. Apple wameona wasogeze karibu/kitu kipya kwa wengine vikatuni vipya lakini kwa wale ambao wanatumia iPhone X watakuwa wameshaona vikatuni hivyo ambavyo vinaweza kufanya kitu fulani (animated).
Kuruhusu programu nyingine ambazo sio za Apple. Ni kama mwanzo wa kufungua milango kwa programu nyingine ambazo Apple hawazimiliki, Google Maps inaweza kutumia vizuri kabisa kwenye Apple Car Play ambayo ilikuwa na mapungufu yake.
iOS 12 inakubali kuanzia kwenye iPhone 5s na kuendelea, iPad Mini 2, iPad Air na kuendelea lakini pia kwenye iPod ya kizazi cha 6.
Hivi sasa toleo lililotoka ni la majaribio kwa waundaji wa Apple walisajiliwa tu na baada ya kufanya malipo, Juni 26 (toleo la majario kwa wote) na mwezi Sept ndio toleo rasmi la iOS 12 litatoka.
Vyanzo: The Guardian, Mac World, TechRadar
One Comment
Comments are closed.