Kampuni ya Apple wamekubali kuna tatizo katika programu tumishi yao maarufu ya FaceTime. App ya FaceTime inaanza kurusha kinachosikika kabla mtumiaji wa iPhone hajapokea simu.
Tatizo hili maarufu kwa jina la kiteknolojia kama ‘bug’, limegunduliwa na watu wengine tuu na sio Apple wenyewe.
App ya FaceTime inafanya kazi kama app ya WhatsApp ila yenyewe inamilikiwa na Apple na inakuja kwenye vifaa vyote vinavyotengenezwa na Apple kama iPhone, iPad na kompyuta/laptop za Mac.
Nini kinatokea?
Kinachotokea ni kwamba kama mtumiaji A wa app ya FaceTime akimpigia mtumiaji B kupitia app hiyo; ikishaita tuu, kabla mtumiaji B hajapokea basi tayari yule aliyepiga ataanza kusikia mazungumzo/sauti kutoka kwa mtumiaji B.
Pia kuna wachunguzi waliosema kuna data za video pia zinarushwa kwenye baadhi ya simu.
Suala la usalama wa data na faragha ya watumiaji wa vifaa vya elektroniki ni jambo nyeti sana kwa mataifa yaliyoendelea na suala limeleta aibu kubwa kwa kampuni ya Apple ambao hujisifia mara zote ya kwamba ndio wana programu endeshaji (iOS & Mac OS) salama zaidi kuliko wengine wote.
Kwa sasa Apple wamekubali uwepo wa tatizo hilo na kuamua kusitisha huduma ya FaceTime kwenye baadhi ya mambo kama vile simu za makundi (Group Calls). Pia wametoa ahadi ya kuleta sasisho jipya la app ya FaceTime ndani ya siku chache, toleo hilo litaondoa kabisa tatizo hilo na pia kuboresha usalama kuzuia tatizo kama hilo kutokea tena ndani ya app hiyo.