Kampuni ya mawasiliano ya simu ya Airtel Tanzania imetangaza kujiunga na mfumo mpya wa kielektroniki wa malipo serikalini uitwao GePG (Government Electronic Payment Gateway system).
Akitoa taarifa hiyo kwa waandishi wa habari, Mkurugenzi wa masoko wa Airtel Tanzania, Bw. Isack Nchunda amesema mfumo huo utatoa suluhisho la kufanya malipo kuwa rahisi ya papo kwa papo kupitia huduma ya Airtel Money.
Mfumo huo ni salama, rahisi na nafuu na wamedhamiria kuendelea kuhudumia wateja kwa ubora wa hali ya juu kwa kuongeza idadi ya mawakala wa Airtel Money ambao kwa sasa wanakadiriwa kuwa zaidi ya 55,000 nchini kote.
Kupitia mfumo huo, wateja wa Airtel Money sasa wataweza kulipia malipo ya huduma mbali mbali pamoja na tozo za serikali mahali popote kutoka kwenye simu zao kama vile ushuru, karo na malipo mengine yoyote.