Kampuni ya ndege ya Airbus ya nchini Ufaransa imepata mkataba mkubwa zaidi kuwahi kupatikana kutoka kwa mnunuaji mmoja wa ndege. Wamepata mkataba wa kutengeneza ndege 430 kwa dola bilioni 49.5 za Kimarekani.
Shirika moja la uwekezaji linalokwenda kwa jina la Indigo Partners la nchini Marekani litalipa pesa hiyo ambayo ni zaidi ya Tsh Trilioni 111.
Mkataba huo utahusisha ndege za familia ya A320neo, ambazo ni ndege za kisasa na zinazosifika sana katika suala la utumiaji wa mafuta – zinakula mafuta machache na huku zikiwa na utendaji mzuri.
Oda hii imeweka rekodi: Ndio oda ya ndege nyingi zaidi kuwahi kuwekwa na mnunuaji mmoja.
Shirika la Indigo Partners linamiliki asilimia flani katika mashirika ya ndege ya Volaris Airlines (nchini Mexico) na Wizz Air (Nchini Hungry). N pia shirika linaumiliki mzima katika mashirika ya ndege ya Frontier Airlines (nchini Marekani) na JetSMART Airlines (nchini Chile).
Mgawanyo wa ndege hizo, 273 zitakuwa za A320neos na 157 zitakuwa jamii ya A321neos;
- Wizz Air: 72 za A320neo na 74 za A321neo;
- Frontier Airlines: 100 za A320neo na 34 za A321neo;
- JetSMART: 56 za A320neo na 14 za A321neo;
- Volaris: 46 za A320neo na 34 za A321neo.
Ndege hizo zitaingizwa katika mashirika hayo, uamuzi wa kuweka oda moja unasaidia kushusha gharama.
Kwa kipindi chote cha mwaka huu shirika la utengenezaji ndege la Boeing ndilo lilikuwa linaongoza kwa kiasi kikubwa katika mauzo na hivyo mkataba huu unawaweka Airbus katika eneo nzuri kwenye ushindani – hali isipobadilika inaweza wafanya kuwa namba moja kwa oda za ndege kwa mwaka huu.
Mkataba (MoU) kati ya Indigo Partners na Airbus umefanyika katika maonesho ya kimataifa ya ndege yanayoendelea huko Dubai.
Vyanzo: CAPA na tovuti mbalimbali
(Masahihisho: Mwanzo tulikosea na kuandika Airbus ni ya nchini Marekani, Boeing ndiyo ya nchini Marekani)